6/recent/ticker-posts

DC SAMIZI ATUMIA MKUTANO WA WADAU WA MAJI SHINYANGA KUZINDUA KAMATI ZA MALALAMIKO

Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Johari Samizi akizungumza wakati wa mkutano wa wadau wa maji wilayani Shinyanga.


Na Mwandishi wetu - Shinyanga
Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini RUWASA wilaya ya Shinyanga wameendesha mkutano mkuu wa nusu mwaka wa wadau wa maji ulioambatana na uundaji wa kamati za malalamiko.

Mkutano huo umefanyika leo Mei 26, 2023 kwenye ukumbi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.


Mkutano huo uliowakutanisha wadau wa maji kwa lengo la kujadili masuala mbalimbali ikiwemo uwasilishaji wa takwimu za CDMT na taarifa za fedha, usimamizi wa fedha na upangaji bei, ubora wa maji na utiaji dawa ya Chlorine, usajili wa CBWSO na utaratibu wa kutatua malalamiko katika wilaya pamoja na majadiliano.


Akitoa taarifa ya Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini RUWASA wilaya ya Shinyanga meneja wa RUWASA wilayani humo Mhandisi Emael Nkopi amesema miongoni mwa majukumu makubwa ya RUWASA ni kupanga, kusanifu, kujenga miundombinu ya maji, kusimamia na kufanya matengenezo kwa kushirikiana na vyombo ya watumia maji ambapo kwa sasa hali ya upatikanaji wa maji kwenye wilaya ya Shinyanga sawa na asilimia 72.3.


“Hali ya upatikanaji wa huduma ya maji kwa sasa imefikia takribani watu 338,962 kati ya watu 468,611 sawa na asilimia 72.3 ya watu wote waishio vijijini idadi hii ya watu ni kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 na hii imechangiwa na uwepo wa miundo mbinu ya maji ya bomba pamoja na visima vinavyutumia pampu ya mikono kwenye maeneo ambayo bado haijafikiwa na miundombinu ya bomba”, amesema Mhandisi Nkopi.


Awali akifungua mkutano huo Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Ngassa Mboji amewapongeza Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini RUWASA wilaya ya Shinyanga kwa kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi wa vijijini kwani kwa sasa hali ya upatikanaji wa huduma ya maji vijijini imezidi kuimarika.


Akizindua kamati za malalamiko mkuu wa wilaya ya Shinyanga Johari Samizi amesema serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo kwa lengo la kuhakikisha wananchi waishio maeneo ya vijijini wanafikiwa na huduma hiyo ya maji na kuwataka viongozi kushirikiana kwa pamoja katika kufanikisha miradi ya maendeleo.


“Kwanza niwapongeze RUWASA wilaya ya Shinyanga kwa kuona umuhimu wa kuandaa mkutano huu wa kukutana na wadau wa maji ili kujadili mustakabali wa maendeleo ya huduma ya maji vijijini, nitumie fursa hii kuwasihi viongozi wote katika maeneo yetu kushirikiana kwa pamoja na si kukwamisha shughuri za kimaendeleo”,amesema.


“Ni matarajio yetu ifikapo 2025 vijiji vyote vitakuwa vimefikiwa na maji, niwaelekeze kila mmoja kwa nafasi zenu kwenda kutekeleza yale yote ambayo tumekumbushwa kupitia mkutano huu ili yaweze kuleta tija ya utekelezaji wa huduma ya maji vijijini”, ameongeza Dc Johari Samizi.








Julieth Payovela Meneja wa RUWASA Mkoa wa Shinyanga akizungumza wakati wa mkutano na wadau wa maji.
Mhandisi Emael Nkopi Meneja wa RUWASA akisoma taarifa ya Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini RUWASA wilaya ya Shinyanga

Wadau wa maji wilayani Shinyanga wakati wa mkutano

Post a Comment

0 Comments