6/recent/ticker-posts

MKURUGENZI MKUU WA NSSF: DHAMIRA YA SERIKALI YA AWAMU YA SITA NI KUHAKIKISHA WANANCHI WALIOJIAJIRI WANANUFAIKA NA HIFADHI YA JAMI

 

*Awapongeza wananchi kwa muitikio wa kujiunga na kuchangia ili kujiwekea akiba kwa maisha bora ya sasa na ya baadaye kupitia kampeni ya NSSF Star Mchezo

Na MWANDISHI WETU,

Arusha. Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Bw. Masha Mshomba, amesema katika Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imetoa fursa kwa Wananchi Waliojiajiri kujiunga na kuchangia NSSF ili wanufaike na huduma na mafao mbalimbali yanayotolewa.

Bw. Mshomba amesema hayo tarehe 7 Machi, 2025 katika soko la Kilombero, Jijini Arusha, wakati akizungumza na Mastaa wa Mchezo wa NSSF waliojiajiri ambao ni wakulima, wafugaji, wavuvi, wachimbaji wadogo wa madini, machinga, bodaboda, wasani mbalimbali, biashara nyingine ndogo ndogo (wasusi, wachuuzi wa masokoni, mamalishe na baba lishe).

"Kwa muda mrefu Mastaa wa Mchezo wa NSSF ambao ni wananchi waliojiajiri walikuwa hawanufaiki na hifadhi ya jamii kwa kujiwekea akiba, lakini Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ilitoa nafasi kwa Wananchi waliojiajiri kujiunga na kuchangia NSSF ili wanufaike na mafao yote yanayotolewa pamoja na mafao la matibabu," amesema Bw. Mshomba.

Amempongeza Rais Mhe. Dkt. Samia kwa kutoa nafasi kwa Wananchi Waliojiajiri kujiunga na kujiwekea akiba kwa ajili ya maisha yao ya sasa na ya baadaye.

Bw. Mshomba ametumia fursa hiyo kuwasihi wananchi waliojiajiri kujiunga kwa wingi NSSF ili iweze kuwahifadhi wanapopata majanga kama ya uzee, maradhi na ulemavu ambapo kwa wanaojiunga na kuchangia NSSF itakuwa Staa wa Mchezo wa baadaye kwa kuwapa mafao na huduma nyingine.

Amesema dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ni kuhakikisha wananchi waliojiajiri wananufaika na hifadhi ya jamii kwa kujiunga na kuchangia NSSF ambapo umewekwa utaratibu mzuri kwani huko huko waliko wakibofya *152*00# wanaweza kujiunga na kuchangia kidogo kidogo kwa siku bukubuku, kwa wiki, kwa mwezi au muhula.

Amewashukuru Mastaa wa Mchezo wote ambao wamenufaika na elimu ya hifadhi ya jamii na kuamua kujiunga na kuchangia kwa maisha bora ya sasa na ya baadaye.

Bw. Mshomba amesema lengo la NSSF ni kuhakikisha wananchi waliojiajiri popote walipo wanapata elimu ya hifadhi ya jamii, wanajiunga na kujiwekea akiba kwani jambo hilo linaenda kuondoa umasikini nchini.

Awali, Makamu Mwenyekiti wa Soko la Kilombero, Bw. Rajabu Hassan,

ameishukuru Serikali kupitia NSSF kwa kufikisha elimu ya hifadhi ya jamii kwa Wananchi Waliojiajiri ili waweze kujiunga na kuchangia kwa ajili ya kujenga maisha bora ya sasa na ya baadaye.

Kwa upande wake, Bw. Gabriel Silayo, Mkurugenzi wa Uwekezaji, Mipango na Miradi, amewahamasisha wananchi waliojiajiri kutumia fursa ya kampeni ya NSSF Staa wa Mchezo kujiunga na kuchangia ili wanufaike na mafao yanayotolewa na NSSF.

NSSF STAA WA MCHEZO, HIFADHI SCHEME - HIFADHI YA JAMII KWA WOTE.




Post a Comment

0 Comments