6/recent/ticker-posts

DKT.MPANGO AZINDUA TAWI LA NMB CHANIKA NA KINYEREZI, AIPONGEZA BENKI YA NMB KWA KUFIKISHA HUDUMA KARIBU NA WANANCHI

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango amesema kufunguliwa kwa matawi ya Benki karibu na wananchi kutasaidia kuondokana na wakopeshaji binafsi maarufu kama kausha damu ambao licha ya kutoza riba kubwa, wananyanyasa na kutweza utu kwa vitendo vya ukamataji mali za wadaiwa. 

Makamu wa Rais amesema hayo mara baada ya kuzindua Tawi la Benki ya NMB Chanika na Tawi la Benki ya NMB Kinyerezi Jijini Dar es Salaam ambapo amesema uzinduzi wa matawi hayo ya Benki utachangia maendeleo ya Taifa kwa kulipa kodi mbalimbali na kutoa ajira za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja.

 Hali kadhalika, amesema tawi la Benki hiyo litawezesha kufanyika kwa usalama zaidi wa miamala mbalimbali kama vile malipo ya bili za maji na umeme, ada za shule na mauzo ya bidhaa mbalimbali.

 Makamu wa Rais ametoa wito kwa Benki ya NMB kuendelea kushiriki katika kutatua changamoto mbalimbali za kijamii ikiwemo katika sekta ya Afya na Elimu. Amesema uwajibikaji kwa jamii ndio msingi imara wa mahusiano bora na yenye tija kati ya benki na jamii. 

Aidha ameongeza kwamba kwa kuendelea kuongeza idadi ya mawakala kutasaidia katika kuzalisha ajira kwa vijana ambao ndio wadau wakubwa huduma hizo. 

Vilevile, Makamu wa Rais amesema ni vema kuelekeza nguvu zaidi katika kukuza elimu na uelewa kuhusu masuala ya fedha ambao umeonekana kuwa mdogo miongoni mwa wananchi.

 Ametoa wito kwa Benki ya NMB kwa kushirikiana na Benki Kuu ya Tanzania na Umoja wa Mabenki kubuni programu na mikakati zaidi ya kuongeza elimu kwa Watanzania, hususan kwa wale waishio vijijini. 

Amesema ni muhimu kuangalia namna bora ya kupunguza gharama za huduma za kibenki za kidijiti ambazo baadhi zinaonekana kuwa kubwa na hivyo kukinzana na lengo la Taifa kupunguza matumizi ya fedha taslimu ili kurahisisha malipo, kuchochea matumizi na kuipunguzia Serikali gharama za kutengeneza sarafu.



Post a Comment

0 Comments